Hosea 4:6

Sunday, February 3, 2013

Kila wakati ntakua natupia neno ambalo kichwa chake cha habari ni Hosea 4:6 linasema "Watu wangu wanaangamia kwa kukosa maarifa" Mungu alishatupatia funguo za kufungulia kila kitu tunachotaka, lakini wengi wamekua wakiendelea kuangamia kutokana na kutokuwa na ufahamu kuhusu mambo kadha wa kadha. Ambapo imewapelekea watu wengi kuomba bila kupata majibu kwasababu hawatumii funguo hizo.



Mimi sio mshauri wa ndoa ila ntatumia mfano huu wa ndoa; Katika ndoa, watu wengi wamekua wakitafuta suluhisho la ndoa zao hawajapata, wengine wametafuta ushauri kwa watumishi mbalimbali lakini hakuna mabadiliko, nakuambia utaomba mpaka magoti yako yaote sugu, utaenda kuomba ushauri kwa washauri wa ndoa hata wa kimataifa ila suluhisho huwezi pata kama wewe mwenyewe hujasimama katika nafasi yako, hutekelezi wajibu wako. Kuombea ndoa yako ni muhimu lakini je, wewe unatimiza maagizo aliyokupa Kristo kama Mume/Mke? 

KWA WANAUME funguo hii hapa, Waefeso 4:25 Enyi waume, wapendeni wake zenu, kama Kristo naye alivyolipenda Kanisa, akajitoa kwa ajili yake. Maana yake hapa ni kwamba Kristo alipenda kanisa pamoja na mapungufu yake yote, watu wanamuudhi lakini akaendelea kulipenda na hakuangalia mapungufu yaliyokua katika kanisa... na hata waume wanatakiwa kuwapenda wake zao hivyo hivyo jinsi walivyo na tabia zao na kila mapungufu yao kama Kristo alivyolipenda kanisa. Kumbuka Kristo hakuwa analalamika, au anagombana na kanisa, ila kwa kila jambo alikua anaonya kwa hekima ya hali ya juu na kwa upole, sasa wewe Mume, je, unavyoishi na mkeo unafuata neno hili? Kumbuka chochote unachotaka kufanya kwa mke wako,jiulize, je, hivyo ndivyo Kristo alivyokuwa anafanya kwa kanisa? au uko nje ya mstari? Ukishaoa wajibu wako ni kumpenda mke wako mpaka kifo kitakapowatenganisha.

Kwa wake; Waefeso 5:22 Enyi wake watiini waume zenu kama kumtii Bwana wetu. Wanawake nao wanaambiwa kuwatii waume zao kama kumtii Kristo, unajua maana ya kama kumtii Kristo? Huwa unamtiije Kristo? hivi kama Kristo akija mbele yako akikuambia jambo hata kama umeona kama amekuonea utajibizana naye? Hapa inamaanisha hata kama mume amekuudhi, unatakiwa umtii tu... umheshimu tu, kwasababu hilo ni agizo tulilopewa na Mungu. Tuache tabia ya kusema nimevumilia vya kutosha, ukishaolewa wajibu wako ni kumtii mume wako mpaka kifo kiwatenganishe.

Kama wewe hujasimama katika nafasi yako ipasavyo, badala ya kuomba Mungu aponye ndoa yako, omba kwanza Mungu akusaidie uweze kutimiza agizo la Kristo alilokupa kuhusu ndoa.

Hii iwe fundisho kwa wale ambao hawajaoa wala kuolewa, waweze kuwa makini na waombe Mungu sana aweze kuwapa wa kufanana nao ambao wataweza kuvumiliana na kuchukuliana katika madhaifu yao.
Somo Litaendelea